Tundu Lissu na Mhariri wa Mawio kizimbani Leo Kwa Tuhuma za Uchochezi

Serikali itawafikisha Mahakama ya Kisutu leo, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu na mmiliki wa gazeti lililofungiwa la Mawio, S... thumbnail 1 summary
Serikali itawafikisha Mahakama ya Kisutu leo, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu na mmiliki wa gazeti lililofungiwa la Mawio, Simon Mkina kwa kuandika habari za uchochezi.

Mkina alisema baada ya kuripoti Kituo Kikuu cha Polisi kuwa kwa mara ya kwanza watafikishwa mahakamani.

“Nimekuja kama ilivyo amri kufika hapa kila siku asubuhi, ila nimeambiwa kesho ( leo )  tunatakiwa kufika mahakamani na wenzangu,” alisema Mkina.

Katika kesi hiyo, atakuwapo pia mhariri na mwandishi wa habari iliyosababisha kufungiwa, Jabir Idrisa pamoja na mchapishaji wa gazeti hilo.

Lissu ameunganishwa katika kesi hiyo kwa madai ya kutoa kauli za uchochezi zilizoandikwa kwenye gazeti hilo.

Pamoja na Gazeti la MAWIO kufungiwa Januari mwaka huu baada ya kudaiwa kuandika habari za uchochezi zilizohusu mgogoro wa kisiasa visiwani Zanzibar ikiwa na kichwa cha habari ‘Machafuko yaja Z’bar’ katika toleo lake la 182 la Januari 14-20, 2016, bado serikali inawang’ang’ania.

Akizungumza na wanahabari Mkina alilaumu kitendo cha polisi kukamata hadi watoa maoni wa gazeti.

Mkina alisema, serikali inabana uhuru wa habari pia kunyima fursa ya kuikosoa hata kama imefanya mabaya.